Pages

Friday, January 3, 2014

hizi ni salamu za mwaka mpya 2014 kutoka kwa mtanzania wa kawaida kwa wana Kibondo na Kakonko



Awali ya yote napenda kumshukuru mwenyezi Mungu mwingi wa rehema , muumba mbingu na dunia kwa kuweza kunifikisha salama katika mwaka huu wa 2014 nikiwa mwenye afya njema. Pia nichukue fursa hii kuwapa pole wote walioanza mwaka huu wa 2014 wakiwa na matatizo mbali mbali kama magonjwa  n.k. Pia wale wote waliotangulia mbele za haki napenda kuchukua fursa hii kuwaombea kwa Mwenyezi Mungu mwingi wa huruma aweze kuwasamehe madhambi yao na kuwalaza mahala pema peponi amina.
Ndugu zangu wanakibondo na kakonko, mimi kama mzaliwa wa kibondo katika kijiji cha Mugunzu nina kila sababu za kuwapa salamu zangu za mwaka mpya wa 2014 kwani ni mwaka ambao una maana sana kwetu wananchi wa kibondo na kakonko. Nasema ni mwaka wenye maana sana kwetu kwasababu ni mwaka ambao nchi yetu inategemea kuwa na uchaguzi wa serikali za mitaa( uchaguzi wa madiwani), hivyo ningependa kuzungumza nanyi japo kidogo na kutoa mtizamo wangu katika Nyanja mbalimbali kama kisiasa,kijamii, afya elimu n.k.
1.UCHAGUZI WA SERIKALI ZA MITAA.
Ndugu zangu kama awali nilivyosema nchi yetu inategemea kuingia kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa mwaka huu wa 2014, hivyo sisi kama wananchi wa kibondo na kakonko inabidi tuwe makini sana katika uchaguzi wa madiwani ambao watakuwa makini katika kuzisimamia halmashauri zetu za wilaya ya kibondo na kakonko.
Kwa nijuavyo mimi diwani ni muhimu sana zaidi ya Mbunge lakini wengi wetu tunaamini kuwa Mbunge ndio ambaye anakazi kubwa ya kuleta maendeleo ya jamii husika, sio kweli ndugu zangu, madiwani ndio wenye umuhimu sana katika utendaji na usimamizi wa shughuli za maendeleo, kwani madiwani ndio ambao tupo nao kila siku katika kata zetu na tunajumuika nao katika shughuli mbalimbali za kila siku hata kero zetu wao wanazijua vizuri kuliko wabunge kwasababu nao ni moja ya waathirika wa kero hizo. Hivyo basi kutokana na dunia ya sasa kuwa imebadilika inabidi tuwe makini katika kuchagua madiwani wenye uwezo na elimu nzuri ili waweze kutusaidia kuzisimamia halmashauri zetu ambazo zimekua tatizo katika utendaji na usimamizi wa fedha za miradi ya maendeleo. Vijana wenzangu ambao tumebalikiwa kupata elimu japo kidogo tujitokeze kugombea hizi nafasi za udiwani kwani kuendelea kuwaachia watu wenye elimu ya darasa la saba ni kuendelea kuiingiza jamii yetu katika lindi la umasikini. Siwadhalau au kuwabeza watu wenye elimu ya darasa la saba, lahasha ila naamini kuwa dunia ya leo ya sanyansi na teknolojia tunahitaji watu ambao watakua na uwezo wa kupambanua mambo mbalimbali kwa undani zaidi na sio ilimradi kukaa na kupokea posho za vikao.
Vijana wenzangu wengi wetu tunawaza sana UBUNGE na kusahau UDIWANI ni wakati sasa wa kuugeukia udiwani ili tuweze kuwa na Halmashauri zilizo bora na za mfano. Kwani tukiwa na Mabaraza ya MADIWANI yaliyo na watu wenye elimu nzuri wataweza kuhoji na kusimami fedha za maendeleo ya wilaya zetu ambazo watendaji wasio waaminifu wamekuwa wakizitafuna.
2.SIASA ZA UDINI NA MAJI TAKA.
Ndugu zangu wanakibondo na Kakonko, tumesikia mengi na kuona mengi katika uchaguzi mkuu uliopita wa 2010 na uchaguzi wa wawakilishi katika mabalaza ya katiba 2013. Inaniuma sana na kusikitika sana kuona Kibondo na sisi tumeanza kuingia katika siasa hizi za kidini, matusi na uzushi. Kuendeleza siasa za namna hii ni kuiingiza jamii yetu katika migogoro mikubwa na kupelekea chuki, uhasama . na uvunjivu wa amani katika wilaya zetu. Tunajisahau kuwa hizi dini tumezipokea tu na hao waliotuletea hizi dini hata wahazifuati kama sisi waafrika tunavyozifuata. Hivyo nachukua fursa hii kuwaomba wanakibondo kutorudia kosa lile lililojitokeza katika uchaguzi wa 2010 na uchaguzi wa wawakilishi wa mabalaza ya katiba. Mimi binafsi siamini kama kiongozi akitoka dini fulani ndio anaweza kuniondolea kero zinazonikabili kuliko kiongozi aliyetoka dini nyingine, bali naamini kiongozi yoyote ambaye anauwezo wa kiuongozi bila kuangalia dini yake ndio anaweza kunitatulia kero zangu. Hivyo huu mtego wa udini inatupasa tuweze kuukwepa haraka sana na atakayekua anafanya siasa za udini tumkanye mapema sana na tumnyime kura zetu kwani huyo hatufai katika wilaya yetu na Taifa kwa ujumla.
Pia kibondo tumekuwa na siasa za chuki majungu na fitna bila sababu yoyote, ni wakati wa kuacha hizi siasa ambazo matokeo yake ni kuchukiana na mwisho wa siku kuuana. Wapo vijana wengi kibondo wanatumiwa na wanasiasa bila wao kujua au wanajua na kupelekea kupandikiza chuki kwa vijana wenzao. Inatupasa tutambue kuwa siasa sio uaduni hata pale tunapotofautiana kimtizamo inabidi tuvumiliane. Na kutokana na hizo tofauti za kimtizamo na kimawazo ndipo tunapopata mawazo mazuri ya kujenga na kutuletea maendeleo. Mtu akipinga wazo lako sio kusema wewe ni mjinga au wazo lako ni la hovyo, tukumbuke kwambia binadamu tunatofautiana sana kifikra.
3. ULIPUAJI WA MIRADI YA MAENDELEO.
a) .Mwaka jana nilikua Kibondo na kuona ile stendi ya mabasi wenyewe tunaiita STENDI MPYA, ukweli nilitamani kulia kwani stendi ile ni ya hovyo sana na sijui imegharamia shilingi ngapi.  Stendi ile haina miundombinu kabisa ya maana hata kituo cha polisi sina hakika kama kipo pale yani ipoipo tu , zaidi niliona kokoto nyekundu ndo zilizo mwagwa pale. Ni wakati wa kusema hapana kwani tunaibiwa mchana kweupe na sisi tunaona. Nilijiuliza maswali mengi sana ila sikuweza kupata jibu mpaka leo sina jibu. Nashindwa kuamini kama baraza la madiwani limekubaliana na ujenzi ule wa stendi ! Au mwezi wa 3 mwaka jana ndo ilikua awamu ya kwanza ya ujenzi wa stendi ya wilaya ? sina jibu mpaka sasa kwani nipo mbali. Ndugu zangu ndo maana nasema tuna kila sababu ya kuchagua madiwani wenye elimu na uwezo wa kuhoji na kuisimamia halmashauri bila woga kwani kwa mwendo huu kamwe hatuwezi kusonga mbele na kufikia ile nchi ya ahadi,  tutaendelea kuwa wilaya ya mwisho kimaendeleo. Niwakati wa kuamka sasa na kusema hapana kwa watendaji wabovu wa Halmashauri.
b). Ilikua mwaka jana nilisikia kwamba kiongozi wa mbio za mwenge kitafa alizindua ujenzi wa uwanja wa mpira wa wilaya maarufu kama uwanja wa Taifa,kinachonishangaza mpaka leo hii sijasikia taarifa kuwa ujenzi umeshaanza zaidi naona picha kupitia facebook vijana wetu wakiendelea kucheza kwenye uwanja uliojaa kokoto na mawe makubwa bila kuhofia kuumia uwanjani. Kweli nimeamini sisi  watanzania tunaishi sana kwa mazoea. Haya yote yanatokea ikiwa madiwani wapo na Mbunge, tena mbunge huyu ni kijana na yeye tumecheza wote kwenye uwanja huo miaka ya 1999 na 2000 ikiwa kiwanja hicho kipo hivyohivyo. Tafadhari wahusika simamieni pesa hizo za miradi ipasavyo.

4.FURSA ZA KIUCHUMI .
a).Kibondo ni moja ya wilaya ambazo zilitakiwa ziwe zimepiga hatua kiuchumi kwa kuangalia geographic position. Kibondo tumepakana na nchi ya burudi na tuna mpaka wa MABAMBA NA MUHANGE, tumeshindwa kutumia fursa hii kibiashara , ni wakati sasa kwa wananchi wa  kibondo kuamka na kuitumia hii fursa ya mipaka kufanya biashara na nchi ya Burundi ili tujikomboe kiuchumi. Tufuate taratibu za nchi zote mbili kisha tuanze biashara. Vijana wenzangu fursa ndio hii, tuache kukaa vijiweni kuanzia asubuhi mpaka jioni tukipiga polojo zisizokwisha kwani umri unasogea tunazeeka tupo vilevile. Bado vijana tumelala sana, tuunde vikundi vya vijana kisha tuombe mikopo midogomidogo na tuanzishe biashara. Tusiogope kukopa kwani hata hao matajiri wakubwa tunaowajua ukiwafatilia wengi wana madeni, angalizo tu ni kwamba tunakopa pesa ili tufanyie mambo ya kibiashara ila sio tukope pesa kisha tukeshe baa hapo mkopo utauona mchungu. Serikali yenyewe inakopa iweje wewe uogope kukopa!! Amka kijana wa kibondo na jitambue sasa.
b). Tumeshindwa kutumia ardhi yetu nzuri yenye rutuba kwa kilimo chenye tija. Kibondo tumebarikiwa sana kuwa na ardhi yenye rutuba , mito na mabonde mengi ambayo tukiyatumia vizuri tutaweza kunufaika katika kilimo, niwakati sasa wa kuitumia ardhi yetu ambayo ni zawadi tuliyopewa na Mwenyezi Mungu katika kufufua uchumi wetu. Wafanyabiashara wa kibondo nawaomba mkigeukie kilimo kwani kupitia kilimo mtaweza kukuza uchumi wenu na wilaya kwa ujumla pia mtasaidia kuzalisha ajira kwa vijana wengi wa kibondo ambao wengi wanashinda vijiweni.
c). Madini ya chumvi na chokaa, kibondo pia tumebahatika kupata madini ya chumvi na chokaa, ni wakati wa watendaji wa serikali kuwahamasisha wafanyabiashara wakubwa wa Tanzania kuja kuwekeza kibondo katika madini haya ili kuweza kuinua uchumi wa wilaya yetu, mwananchi wa kawaida na Taifa kwa ujumla. Kutokana na kibondo kupakana na nchi ya Burundi kama tutapata kiwanda cha chumvi na simenti wawekezaji wataweza kuuza nje ya nchi kama Burundi, Kongo, Rwanda n.k. Pia wananchi wa kibondo wataweza kujenga nyumba zilizo bora kwani gharama ya sementi itashuka kutokana na uzalishaji kufanyika kibondo. Vilevile wilaya na mikoa ya jirani itaweza kunufaika na viwanda hivi vitakavyojengwa.


5. UHARIBIFU WA MAZINGIRA, UHUJUMU WA MBOLEA ZA RUZUKU NA WIMBI LA UJAMBAZI.
a). Toka wananchi wa kibondo wajikite katika kilimo cha TUMBAKU kumekua na uharibifu mkubwa wa mazingira kwani uoto wa asili umekuwa ukikatwa katika hatua za uandaaji wa mashamba ya tumbaku, misitu pia imekua ikakatwa hovyo ili kupata kuni za kukaushia tumbaku hizo. Serikali kupitia mamlaka husika inatakiwa kuweka sheria kali ili kuweza kuokoa mazingira haya ambayo yanaharibiwa hovyo, pia serikali itoe elimu juu ya mazingira kwa wananchi wanaojihusisha na kilimo hiki naikiwezekana itafute zao mbadala la biashara ili kuokoa mazingira yetu.
b). Kitu ambacho kinaniuma sana ni kuona mbolea ya ruzuku ikihujumiwa na wafanyabiashara mbalimbali wilayani Kibondo kwa kuwahonga wananchi pesa kidogo na wananchi hao kuwauzia vocha za mbolea kwa bei ya chini kisha wao kuwauzia tena mbolea hizo kwa bei ya juu. Mchezo huu mchafu umekua ukifanywa na watendaji wa vijiji wasio waaminifu na waroho wa fedha kwa kuwakandamiza wakulima kwakua wanajua kabisa wakulima wengi ni masikini na wanauelewa mdogo juu ya vocha zinazotoka Serikalini. Hii hali niliiona ndani ya siku tatu nilizokaa kibondo kipindi cha likizo na nilishindwa kuchukua hatua stahiki kwakua nilikua na muda mchache. Sasa ni wakati wa kuwasema hadharani wafanyabiashara hao na hao watendaji wa vijiji wasio waaminifu ili mkono wa sheria uweze kuchukua nafasi yake. Wewe raia mwema na mpenda maendeleo ya kibondo toa taarifa kwa njia ya siri kwenye vyombo vya ulinzi na usalama vya wilaya ili kuweza kumsaidia huyu mkulima ambaye anadhurumiwa na hawa wafanyabiashara.
c). Tatizo la ujambazi bado lipo kibondo.Hili sitalizungumzia sana kwakua sijalifanyia utafiti wa kutosha. Naimani operation kimbunga imesaidia kupunguza ujambazi katika wilaya yetu. Kinachotakiwa ni sisi wananchi wa kibondo kutoa taarifa polisi pale tu tunapomwona mtu ambaye hatumwelewi kwa kufanya hivyo itatusaidia kupunguza au kutokomeza kabisa tatizo hili linalotukabili si kibondo tu bali Taifa kwa ujumla.

Ndugu zangu yapo mengi ningependa nijumuike nanyi katika mwaka huu mpya wa 2014 , lakini acha kwa leo niishie hapa na siku nyingine nikipata nafasi nijaongea mengine kwa ajiri ya maendeleo ya KIBONDO.
Nawatakia afya njema, mafanikio ya kiuchumi katika mwaka huu wa 2014 na Mungu awafanikishie kila lile jema mlilopanga kufanya katika mwaka huu.





HIZI NDIZO SALAMU ZANGU ZA MWAKA MPYA WA 2014 KWENU WANAKIBONDO WENZANGU.
NI MIMI NDUGU YENU,KIJANA MWENZENU NA MTOTO WENU.

NDUHILUBUSA MAPIGANO
MOSCOW, RUSSIA
2014.
ASANTENI SANA.

No comments:

Post a Comment